TANZANITE YAIFUATA ETHIOPIA MECHI YA MARUDIANO
KIKOSI cha timu ya taifa za wasichana chini ya umri wa miaka 20, Tanzanite kimeondoka leo jioni Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Kilimanjaro (KIA) kwenda Ethiopia kwa ajili ya mchezo wa marudano na wenyeji kufuzu Kombe la Dunia Ijumaa Jijini Addis Ababa.
Tanzanite ambayo iliweka kambi ya wiki moja akademi ya Black Rhino, Karatu mkoani Manyara - inahitaji sare katika mchezo huo kufuatia ushindi wa 1-0 kwenye mchezo wa kwanza Jumapili iliyopita Uwanja wa Aman, Zanzibar.
Ikifanikiwa kuitoa Ethiopia itakutana na mshindi wa jumla kati ya Uganda na Ghana, ambao ni mtihani wa mwisho utakaotoa tiketi ya kwenda Costa Rica katika Fainali zitakazoanza Agosti 10 hadi 28, mwaka huu.
Comments
Post a Comment